ASKOFU WA TAG DR. BARNABAS MTOKAMBALI AWATAKA WACHUNGAJI KUJIEPUSHA NA SIASA

WACHUNGAJI wa Kanisa la Tanzania Assemblies of God wametakiwa kuacha kuyafanya makanisa wanayoyachunga kuwa ya kisiasa ili kutunza amani na utulivu katika nchi ya Tanzania.

Askofu wa Kanisa la Tanzania Assemblies of God Dk. Barnabas Mtokambali aliyasema hayo wakati akiliweka wakfu jengo jipya la kuabudia la kimataifa la Calvary Christian Centre la Kanisa hilo katika mji mdogo wa Tunduma mkoani Mbeya Jumatano ya wiki hii.

Akizungumza kwa msisitizo mkubwa Askofu Mtokambali alisema changamoto iliyopo sasa katika nchi ya Tanzania na kanisa kwa ujumla ni kwamba mfumo wa vyama vingi umewashika sana watanzania huku kanisa likiwa katika mpango mkakati.

Askofu Mtokambali katika suala la mfumo wa vyama vingi nchini Tanzania, alisema mchungaji akiegemea katika chama fulani atasababisha amani na utulivu kupotea kwani migongano ya kimaslahi itaingia ndani ya mioyo ya waamini na makundi ndani ya kanisa yatajitokeza hali itakayomfukuza Roho Mtakatifu.

Suala la Mpango mkakati Askofu Mtokambali alisema utaingia doa endapo ndani ya kanisa wachungaji watakuwa wakivutia chama fulani na waliotakiwa kuokoka hawataokoka na mchungaji atatumika kama kizuizi cha watu kusababisha Injili isisonge mbele.

“Wachungaji miongoni katika kanisa letu wamejiingiza katika siasa hali ambayo imeleta magomvi na kupoteza ladha ya kuitwa kanisa la Mungu, hebu fikiria mchungaji anakuwa wa CUF, ama CCM ama CHADEMA au chama chochote cha siasa nchini ikitokea timbwili nini kitatokea baina ya chama chake na vingine ambavyo ndani yake kuna washirika ndani ya kanisa analolichunga” alisema Askofu Mtokambali.

Askofu Mtokambali aliongeza kusema Kanisa la TAG limetoa ruhusa kwa mchungaji yeyote anayetaka kujiingiza katika siasa lakini kwa masharti ya kuachana na kazi ya uchungaji  na kuingia katika siasa.

“ Bila hata fujo mchungaji anaruhusiwa kuja kwa wakuu na kurudisha joho la uchungaji pamoja na kanisa na kwa amani zote tunamwombea ili afanikiwe katika siasa kama ni ubunge au nafasi yoyote ile katika siasa kuliko kufanyia siasa kanisani kwani kanisa haliko kwa ajili ya hayo” alisisitiza Askofu Mtokambali.

Pia alisema Kanisa sio mahali pa kufanyia mambo ya hovyo yenye kupunguza uwepo wa Mungu, na kwamba Mchungaji yupo kama mwamuzi baina ya washirika inapotokea kutokuelewana na pia kuwaongeza ufahamu waamini kuhusu ufalme wa Mungu.

“Mchungaji ni kama mwamuzi uwanjani anapocheza mechi ili kuweka usawa, hivyo mchungaji anatumiwa na Mungu kuweka usawa ndani ya kanisa na kuwanidhamisha wale wanaoleta fujo, hata hivyo Sheria za nchi ya Tanzania hazimruhusu Mchungaji kuwa shabiki wa chama chochote cha siasa” aliongeza Dr. Mtokambali.

Hata hivyo Askofu Mtokambali aliwataka waumini wa makanisa yote ya TAG kuishi maisha ya Utakatifu ili Mungu ainuliwe katika mpango mkakati wa miaka 10 ambao ifikapo mwaka 2018 kanisa liwe na waamini million mbili.

“Maisha ya utakatifu miujiza huja yenyewe, watu huokoka wenyewe kila kitu hufanyika kwasababu Roho Mtakatifu anakuwa pamoja na waaminifu wake” alisisitiza

Katika uzinduzi huo Askofu Barnabas Mtokambali alipokelewa na Mkuu wa Wilaya ya Mbozi Mheshimiwa Gabriel Kimolo ambaye aliwasisitizia waamini wa wilaya hiyo waliokuwepo hapo kuwa wilaya hiyo itaendelea kwasababu ya wacha Mungu.

“ Kama ujuavyo Mbozi imekuwa mahiri sana kwa vitendo vya aibu visivyompendeza Mungu vya mauaji, ushirikina, uchunaji ngozi na kadhalika lakini kuzinduliwa kwa jingo hili kutasaidia watu kumjua Mungu wa kweli na kumrudia yeye” alisema Mheshimiwa Kimolo.

Mchungaji Eliud Kalinga wa Kanisa hilo alisema ataendelea kuwa mwaminifu wa Mungu na kwa Tanzania Assemblies of God kuhakikisha mpango mkakati wa 2009-2018 (Decade of Harvest) unatimia na kuzidi pamoja na watu wa Mungu.

Katika uzinduzi huo kiasi cha milioni 8.5 zilikusanywa zikiwemo ahadi kwa ajili ya kumalizia jengo hilo kwa upande wa madirisha, kwani kiasi cha milioni 16 zinahitajika kukamilisha ujenzi wa madirisha.

Pia kila mshirika alishiriki uwekaji wakfu wa jingo hilo kwa maombi ambayo Askofu Mtokambali aliyaongoza katika ibada hiyo iliyoanza majira ya saa 5:30 asubuhi hadi jioni ya siku hiyo na kuhudhuriwa na watu wa kila dini kutoka maeneo mbalimbali mkoani Mbeya.

Aidha Askofu, Dk. Barnabas Mtokambali alisindikizwa na uongozi wa Jimbo la Kusini Magharibi akiwemo Mlezi Askofu Mwaisabila ambapo kabla ya hapo walikuwa na mazungumzo na mkuu wa wilaya katika ofisi zake katika mji wa Vwawa yakiwa na madhumuni ya kufahamiana zaidi kwani ni mara yake ya kwanza kukutana na Mheshimiwa Gabriel Kimolo.

Katika  ziara mkoani Mbeya, Askofu Mtokambali alitembelea pia maeneo ya Nkanga wilayani Chunya, Mwakaleli- Tukuyu wilayani Rungwe.
Imeandikwa na Johnson Jabir Desemba 14, 2011

Post a Comment

0 Comments