Familia ya Mangi Mkuu yaikabidhi KKKT kitabu cha historia ya kanisa

Themi Marealle mojawapo ya wanafamilia ya Mangi Mkuu Thomas Marealle II OBE akimkabidhi kitabu cha Historia ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Afrika Mashariki 1902-1912, Askofu Mkuu wa Dayosisi ya Kaskazini Dkt. Fredrick Onael Shoo katika hafla fupi iliyofanyika Mjini Moshi Mei 16, 2019. 
Familia ya Mangi Mkuu Thomas Marealle II OBE ya Kilimanjaro imetoa kitabu cha historia ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania  (KKKT), Dayosisi ya Kaskazini kuanzia mwaka 1902 hadi 1912 kwa kanisa hilo.

Katika tukio hilo Askofu Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Kaskazini Dkt. Fredrick Onael Shoo alipokea vitabu zaidi ya 100 vya historia ya kanisa hilo Afrika Mashariki kutoka kwa familia ya Mshumbue Marealle II OBE aliyetafsiri kutoka lugha ya kiingereza hadi Kiswahili.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo ya kumkabidhi iliyofanyika ofisini kwa Askofu Mkuu Dkt. Shoo hivi karibuni, Themi Marealle ambaye ni  miongoni mwa wanafamilia ya Marealle II alisema wameamua kufanya hivyo ili waumini watakaokisoma waweze kujua historia yao.

“Kwa hiyo kitabu hiki ni historia ya KKKT hapa Kaskazini  na tunaomba kukukabidhi kitabu hiki ili waumini na hata watu wengine watakaopata nafasi ya kukisoma wajue historia yao, Baba Askofu nakushukuru sana Mungu akubariki.” alisema Themi Marealle.

Katika hafla hiyo Themi Marealle aliongeza kuwa kitabu hicho kiliandikwa kwanza na wachungaji wawili wa Kijerumani ambao ni Adolphi na Shantz.

“Baba Askofu tumefika hapa kukabidhi kitabu chenye historia ya Kanisa la Kiinjili Kilutheri Tanganyika maeneo ya Kilimanjaro, Arusha, Meru na Pare; kiliandikwa mara ya kwanza na wachungaji wawili Wajerumani  baada ya hapo mheshimiwa Marealle alimwomba mwalimu wa International School Moshi akitafsiri kutoka kijerumani hadi kiingereza naye akakitafsiri kutoka Kiingereza kwenda Kiswahili ili watu wa Kilimanjaro na Tanzania waweze kukisoma,” aliongeza Themi.
Aggrey Marealle akisalimiana na Askofu Mkuu Dayosisi ya Kaskazini Dkt. Fredrick Onael Shoo, katikati ni Themi Marealle.
Kwa upande wake Askofu Mkuu Dkt. Shoo alisifu ujasiri huo na uzalendo wa familia hiyo waliouonyesha kwa kanisa na kwamba ni mfano wa kuigwa.

“Shukrani kwanza kwa familia kwa kupenda kutoa kitabu hiki ambacho ni kizuri sana kwa historia ya kanisa letu kuanzia mwaka ule wa 1902 hadi 1912 huu ni mchango mkubwa sana ambao Mangi Mkuu Thomas Marealle ametuachia, lakini familia kipekee ikaona isibaki na vitabu bali wavitoe sadaka yao kwa kanisa,” alisema Askofu Shoo.

“Napenda kuwashukuru sana kwa sadaka. Ni imani yangu kwamba vitabu hivi vitatumika kwa kuwapatia watu sio kizazi cha sasa tu lakini hata vizazi kinachokuja ufahamu wa historia ya uwepo wa kanisa letu la Kiinjili la Kilutheri hasa katika eneo hili la Kaskazini,” aliongeza Askofu Shoo.

Familia hiyo imetoa kitabu hicho chenye kurasa 207 kinachojulikana, “HISTORI YA KANISA LA KIINJILI LA KILUTHERI AFRIKA MASHARIKI 1902-1912 (Kilimanjaro, Arusha, Meru na Pare).”

Mangi Mkuu Thomas Marealle II OBE alitafsiri kitabu hicho akiwa na msaidizi wake Rusk Shirima Kishimba; ambapo Kitabu hicho kiliandikwa kwa mara ya kwanza kwa lugha ya Kidachi (Kijerumani). Baada ya hapo kilitafsiriwa kutoka Udachi hadi kiingereza na Mhisani Anthony Pyane wa London.

CHANZO: JAIZMELA News
ADDITIONS: MCRCTV

Post a Comment

0 Comments