Pastor Chris, mwanzilishi na Rais wa Huduma ya Christ Embassy (LoveWorld Incorporated)


Desemba 7, 1963 alizaliwa mtumishi wa Mungu, mchungaji na mwandishi wa vitabu raia wa Nigeria maarufu kwa jina la Pastor Chris.

Jina lake halisi ni Chris Oyakhilome ambaye ni mwanzilishi na Rais wa Huduma ya LoveWorld Incorporated maarufu Ubalozi wa Kristo. Makao yake makuu yapo Lagos nchini Nigeria.

Ni mtoto wa kwanza wa familia ya Tim Oyakhilome. Mnamo mwaka 1991 Oyakhilome alimuoa Anita Ebhodaghe  ambaye alizaa naye watoto wawili wa kike.

Mwanamke huyo aliachana na Pastor kwa kesi iliyopelekwa katika Mahakama moja jijini London mnamo Aprili 9, 2014.

Baada ya kutalikiana (wadaawa) iliamuliwa mahakamani hapo kuwa watabeba majukumu ya kuwalea watoto hao wawili.  

Talaka ilitoka Oktoba 6, 2016 baada ya miaka 25 ya wawili hao kuishi pamoja huku kiini kikubwa cha kuachana kwao kikitajwa kuwa ni ‘Tabia zisizovumilika.”

Mnamo Oktoba 6, 2018 binti yake wa kwanza anayefahamika kwa jina la Sharon aliolewa na raia wa Ghana Phillip Frimpong katika harusi ambayo inaelezwa kuwa mama yake hakushiriki.

Mnamo mwaka 2011 jarida la Forbes lilikadiria utajiri wa Oyakhilome kuwa ni kati ya dola za kimarekani milioni 30 hadi 50.

Katika suala la huduma yake Pastor Chris amekuwa akifanya kazi katika nchi mbalimbali zikiwamo Uingereza na Marekani na pia ana vipindi nchini Afrika Kusini na Canada.

Pia Pastor Chris amekuwa akifanya huduma ya uponyaji katika mikutano yake nchini Ghana.

Pastor Chris amekuwa miongoni mwa waanzilishi wa kwanza wa kufanya huduma katika vipindi vya televisheni vinavyoruka toka barani Afrika kwenda ulimwenguni kote.

Mnamo mwaka 2005 aliweka rekodi ya kukusanya watu katika mkutano wa usiku wa Neno la Mungu, tukio ambalo lilipewa jina la ‘Good Friday Miracle Night’.

Takribani watu milioni 3.5 walihudhuria.  Nchini Afrika Kusini alishafanya tukio lililopewa jina la Night of Bliss lililofanyika katika Uwanja wa Mpira wa FNB jijini Johannesburg. 

Pastor Chris amekuwa akifanya huduma yake kupitia mtandao wa Intaneti hususani mitandao ya kijamii katika nchi tofauti.

Mnamo mwaka 2013 aliweka rekodi ya kuwa na wafuatiliaji katika mtandao wa Twitter milioni 1.2 pia milioni 1.9 katika Facebook. Pastor Chris anaendesha mtandao wa kuchati wa KingsChat.

Katika masuala ya uandishi wa vitabu ameandika vitabu vingi vikiwamo ‘Rhapsody of Realities’. Kitabu hicho kimeweka rekodi ya pili duniani kwa kutafsiriwa katika lugha mbalimbali baada ya Biblia.

Pastor Chris alipata udaktari wa heshima kutoka katika vyuo vikuu viwili Ambrose Alli na Benson Idahosa vyote vya nchini Nigeria.

Hata hivyo Pastor Chris amepitia katika changamoto nyingi katika huduma yake ikiwamo mafundisho yake kuhusu ndoa.

Alijikuta akipata upinzani mkali kutoka katika mitandao ya kijamii kuhusu usawa katika ndoa kwa mtazamo wake wa kidini.

Katika mojawapo ya chapisho lake katika ukurasa wa Facebook lililopewa jina la  ‘Who is a Husband and What is his role?’ lilileta ukosoaji mkali ambapo katika ndani yake ilionyesha wanaume ni ‘Masters’.  

Katika hilo Pastor Chris alisema matatizo mengi katika ndoa za Kikristo yanatokana na Mungu mwenyewe kutoweka wazi maana halisi ya kuolewa.

Pastor Chris alisema wanawake wanaamini kuwa wapo sawa katika mapenzi lakini kuwa na mume haimanishi kuwa ni mpenzi wake bali ina maana ya mkuu yaani Master.

Alikaririwa akisema, “ Biblia inasema mwanaume ni kichwa cha mwanamke (1 Kor. 11:3) kwa hiyo unapoolewa unaingia katika mamlaka yake. Na sio kwamba mtakuwa sawa katika mamlaka, licha ya kwanza ninyi nyote wawili ni warithi wa Ufalme wa Mungu.”

Pia Pastor Chris alipata upinzani mkali kuhusu mtazamo wake wa kidini kwenye mapambano dhidi ya VVU/UKIMWI kwa kile alichosema maradhi kama hayo yanaweza kutoweka kwa kukemea kwa Jina la Yesu.


Post a Comment

0 Comments